Kuelekea mchezo dhidi ya Al Masry uenda mashabiki Simba viroho vikawa vinawadunda kutokana na taarifa kwamba nyota
wao, John Bocco na Emmanuel Okwi huenda wakakosekana katika mechi hiyo itakayopigwa Jumatano lakini makocha wa timu wana jambo wamefanya.
Benchi la ufundi chini ya Mfaransa, Pierre Lechantre na Msaidizi
wake Mrundi Masoud Djuma limewapa kazi maalumu wachezaji hao ili
kuhakikisha msimu huu
katika Ligi Kuu Bara wanatimiza lengo lao la kubeba ndoo.
Okwi anayeongoza kwa mabao katika ligi hiyo akiwa na 16, huku Bocco
akiwa nafasi ya tatu na mabao yake 10 wamepewa kazi maalumu ya
kuhakikisha mwisho wa msimu huu mmojawao lazima awe mfungaji bora.
Djuma alisema huwa ana utamaduni wa kukaa kikao cha kati yake na
Lechantre mara baada ya mechi kama walimu kujadili makosa na kasoro
zilizojitokeza ili kuzirekebisha.
“Katika kikao chetu kimoja tulikubaliana na Lechantre kuwapa kazi Okwi
na Bocco kuwa mmoja wao anatakiwa kuwa mfungaji bora msimu, kwani
wakiweza kufanya hivyo watakuwa wanailainisha timu kupata matokeo mazuri
katika kila mechi.”
“Hata mfumo tunaoutumia kwa katika timu yetu unawarahisishia kupata
nafasi nyingi za kufunga Okwi na Bocco na tunashukuru kwa kutuelewana
katika hilo kwani wamefikia nusu ya ambayo tunataka kutoka kwao,”
alisema Djuma.
“Mfumo wetu pia unaruhusu kwa wachezaji wengine kufunga lakini Okwi na
Bocco, hatujawawekea idadi ya magoli ya kufunga lakini tunataka wafunge
zaidi katika ligi na kimataifa,” aliongezea.

Comments