Jamuhuri ya Watu wa China itaendelea kuwa Mshirika mkubwa wa Zanzibar katika harakati za Uimarishaji wa Maendeleo ya Kiuchumi Kibiashara, Miundombinu na Ustawi wa jamii.
Makamu
wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi amesema hayo hapo
Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar wakati alipofanya mazungumzo na
Ujumbe wa Kampuni ya Ujenzi wa Reli Nchini China
{CRCG} ukiongozwa na Mwenyekiti wa Bodi ya Kampuni hiyo Bwana Liu Rongyao.
Balozi Seif alisema jamii
imeshuhudia juhudi za China zinavyozidi kuongezeka katika kuona
Zanzibar inajikwamua katika wimbi la umasikini kupitia kasi za
uimarishaji miundo mbinu.
Aliyapongeza Makampuni mbali
mbali ya China yanayotowa huduma zake hapa Zanzibar hasa yale ya Ujenzi
ambayo kwa kiasi kikubwa yanaendelea kuchangia mabadiliko ya haiba ya
Mji wa Zanzibar katika kipindi kifupi.
Alisisitiza kwamba ukamini wao
katika kutoa huduma hizo ndio unaopelekea kuchaguliwa baada ya kushinda
tenda dhidi ya Makampuni mengine Duniani na zaidi Barani Afrika.
“ Ujenzi wa baadhi ya Majengo
ya Taasisi za Serikali , Mashirika ya Umma na hata miradi ya Jamii ni
ushahidi uliowazi wa juhudi za Makampuni hayo”. Alisisitiza Balozi Seif.
Makamu wa Pili wa Rais wa
Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi aliyahakikishia Makampuni yote yanayotowa
huduma hapa Zanzibar kwamba Serikali itashirikiana nayo kwa lengo la
kuhakikisha yanakamilisha miradi yao kwa wakati uliopangwa.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa
Bodi ya Kampuni hiyo ya Ujenzi wa Reli Nchini China Bwa Liu Rongyao
alisema kwamba Ujumbe wao upo Nchini kukagua Miradi ya Ujenzi
inayosimamiwa na Kampuni hiyo ikiwemo ile ya Makaazi ya Nyumba za
Viongozi na Ofisi za Serikali .
Ujenzi huo unafanywa kwa njia ya Mkopo kutoka Serikali ya Jamuhuri ya Watu wa China.
Mapema
asubuhi Balozi Seif alikutana na Ujumbe wa Jumuiya inayojishughulisha
na Miradi ya Maendeleo ya Kijamii kutoka Nchini Marekani ya Rosenthall
Group.
Bw. Robert alisema mbali ya
ujenzi wa nyumba katika kipindi kifupi unaofanywa na Taasisi yao lakini
pia hutoa Taaluma ya huduma ya kwanza na Biashara mafunzo ambayo
huchukua takriban Wanafunzi 150.
Naye Balozi Seif aliuomba
Ujumbe huo kuangalia zaidi maeneo ambayo wanaweza kuwekeza hapa
Zanzibar kwa nia ya kusaidia Uchumi wa Taifa.
Balozi Seif alisema yapo maeneo
mengi yaliyopewa kipau mbele katika kuongeza kasi ya maendeleo
akiyataja kuwa ni pamoja na Utalii, Kilimo, Huduma za Umme na Miundo
mbinu.
Wakati huo huo Makamu wa Pili
wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif alikuwa na Maungumzo na Balozi wa
Shirikisho la Ujerumani Nchini Tanzania Bwana Klaus Peter Brandes.
Bwana Peter alifika Ofisini kwa
Balozi Seif Vuga Mjini Zanzibar kumtambulisha rasmi Balozi Mdogo wa
Shirikisho la Ujerumani atakayefanya kazi hapa Zanzibar Bwana Hans
Dieter Allgaier.
Balozi Seif amemuahidi Bwana
Allgaier kwamba Serikali itajitahidi kumpa mashirikiano zaidi ili kuona
jukumu alilokabidhiwa na Nchi yake linafikiwa.
Makamu
wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akiwa katika picha ya
pamoja na Ujumbe wa Jumuiya inayojishughulisha na Miradi ya Maendeleo
ya Kijamii kutoka Nchini Marekani ya Rosenthall Group pamoja na
Washirika wao hapa Tanzania
Comments