Skip to main content

Rais wa Zanzibar Dk. Sheina Atoa Siku Tatu za Maombolezo Zanzibar.





Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imetangaza siku tatu za maombolezo kuanzia Julai 19 hadi Julai 21 kufuatia maafa ya ajali ya Meli ya Mv. Skagit iliyozama karibu na Kisiwa cha Chumbe Zanzibar.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,Dk. Ali Mohammed Shein akitangaza maombolezo hayo, alisema bendera zote zitapepea nusu mlingoti na kwamba shughuli za sherehe na burudani zimefutwa kwa muda wa siku tatu za maombolezo.
Dk. Shein alisema shughuli za Serikali zitaendelea kama kawaida. Katika taarifa yake aliyoitoa Ikulu usiku wa kuamkia Julai 19, Rais Dk Shein amewahakikishia wananchi na hasa waliopoteza jamaa zao kuwa Serikali itabeba gharama zote za mazishi na pia kugharamia huduma za matibabu kwa majeruhi.
“Nimesikitishwa sana na msiba huu, Katika wakati huu si vema tukaanza kulaumiana jambo la muhimu hivi sasa ni kuokoa maisha ya watu” Alisema Rais Dk. Shein.
Mbali ya taarifa hiyo, Rais Dk Shein aliungana na wananchi, viongozi wa Serikali, vyama vya siasa, Viongozi wa dini katika kutambua maiti zilizofikishwa katika eneo maalum la viwanja vya Maisara Suleiman.
Mbali ya kwenda katika viwanja hivyo, pia alifika katika eneo la bandari ya Zanzibar kufuatilia taarifa za tukio hilo. Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jana lilisitisha shughuli zake kufuatia maafa hayo ambapo wakati wa jioni Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Emmanuel Nchimbi alitarajiwa kufanya majumuisho ya bajeti yake.

Comments