Skip to main content

Gazeti la Mwanachi: Nishati na Madini yawagawa wabunge

KATIBU MKUU AZILIPUA KAMPUNI ZA MAFUTA, ASEMA HAKUNA MGAWO WA UMEME

Waziri wa Nishati na Madini, Pofesa Sospeter 
Muhongo

Mwandishi Wetu

WAKATI baadhi ya wabunge wakitaka kuwachukulia hatua Waziri wa Nishati na Madini, Pofesa Sospeter Muhongo na Katibu Mkuu wake, Eliakimu Maswi kwa madai ya kuiuka sheria ya Ununuzi wa Umma, mtendaji mkuu huyo wa wizara ametupa kombora la ufisadi dhidi ya baadhi ya kampuni za mafuta nchini.

Wanaowatuhumu akina Muhongo na Maswi wanadai kuwa, walikiuka sheria ya ununuzi wa umma kwa kuipa zabuni Kampuni ya Puma Energy ya kununua mafuta ya kuendesha mitambo ya kuzalisha umeme ya IPTL na kuziweka kando kampuni zilizokuwa zimechaguliwa kupitia mchakato halali wa zabuni ya Tanesco.

Suala hilo linahusishwa na kusimamishwa kwa Mkurugenzi Mkuu wa Tanesco, William Mhando kwamba alichukuliwa hatua baada ya kukataa kutii maelekezo ya Wizara.

Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili unaonyesha kuwa kumekuwa na mgawanyiko miongoni mwa wabunge, ambao unaanzia kwenye Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini ambayo hadi sasa hawajaafiki uamuzi wa kuwachukulia hatua viongozi hao.

“Ni kama tumeshindwa kuelewana huko kwenye Kamati, lakini wabunge ndio tumekuwa tukilalamikia ufisadi Tanesco, sasa tunawashangaa wenzetu ambao wameanza kuiandama tena Serikali kwa kuchukua hatua,” alisema mmoja wa wabunge wa CCM.

Mjumbe mwingine ambaye pia ni Mbunge wa CCM alisema kuwa, Muhongo na Maswi walikiuka sheria.

“Tutakuwa tunakosea, tukiruhusu hawa watu wavunje sheria na halafu eti tuwaachie,” alsema mbunge huyo.

Nje ya Kamati hiyo, wabunge bila kujali itikadi zao nao wamegawanyika huku wengine wakitaka viongozi hao wachukuliwe hatua kuhusiana na suala hilo na wengine walisema: “Hakuna kosa walilofanya, waachwe waendelee na kazi.”

Chanzo cha mgawanyiko huo ni sababu zilizotolewa na uongozi wa Wizara ya Nishati na Madini kwamba waliwapa Tanesco fedha za kununua mafuta mazito ili kuiepusha nchi na mgawo wa umeme, lakini wakaelekeza mafuta hayo yanunuliwe Kampuni ya Purma ambako bei ya lita moja ni Sh1,460.

Comments