
Hoja ya kukiondoa kituo kikuu cha
mabasi katikati ya jiji ambayo ilitumiwa na aliyekuwa Mbunge wa Arusha
Mjini, Godbless Lema (Chadema) kujinadi katika kampeni zake za uchaguzi
mkuu ulipita, sasa ametwishwa Meya wa Jiji Gaudence Lyimo (CCM).
Aliyemtwisha zigo hilo ni
Waziri wa Ujenzi Dk. John Magufuli na alifanya hivyo wakati akifungua
mkutano wa wadau wakuu wa Mfuko wa Bodi ya Barabara uliofanyika jijini
hapa juzi.
Magufuli alikuwa akizungumzia
mikakati ya kuondoa foleni inayoanza kulinyemelea jiji la Arusha ambapo
alisema moja ya ufumbuzi ni kuihamisha stendi hiyo ya mabasi.
“Ni vizuri Meya upo hapa,
wekeni mikakati ya kuhamisha ile stendi, hakuna haja ya mabasi yote
yanayokuja Arusha lazima yaingie katikati ya jiji,” alisema na
kuongeza, “tena katika jiji hili mnaweza kuwa na stendi tatu za mabasi
makubwa katika maeneo tofauti kulingana na mahitaji.”
Alitaja maeneo hayo ambayo ni
nje ya jiji kuwa ni kwa mabasi yanayotokea barabara ya Moshi,
yanayotokea Dodoma na Babati na stendi nyingine ni kwa mabasi
yanayotokea barabara ya Namanga.
Comments