Viongozi wa kidini wa Kikiristo na Kiislamu wamesema kuwa wanataka
kufanya mkutano wa dini za imani mbalimbali mwishoni mwa mwaka
kuhamasisha uelewa na kusaidia kuondoa mtindo hasi usiobadilika na usio
sahihi.
Viongozi kumi na watano kutoka makanisa mbalimbali ya kikiristo
walikusanyika huko Wajir tarehe 26 Septemba kujadili kwa ufasaha na
wananchi kuhusu Uislamu na kuhimiza mazungumzo ya heshima na ya amani na
Waislamu katika wilaya hiyo.
Viongozi hao, ambao ni sehemu ya Ushirika wa Wakiristo wa Wajir,
waliitisha mkutano huo kujibu filamu ya utata inayopinga Uislamu,
"Innocence of Muslims", ambayo ilichochea upingaji wenye vurugu katika
nchi kadhaa zenye idadi kubwa ya Waislamu.
Kutokana na mkutano huo, Wakiristo na Waislamu wamepanga kufanya mkutano
wa dini za imani mbalimbali, kwa mujibu wa Mchungaji Eustus Nyagah wa
Kanisa la Pentekoste la Afrika Mashariki huko Wajir. Mkutano huo
unadhamiria kuwaleta watu pamoja kubadilishana mawazo kwa namna ya
heshima na kusaidia kuondoa chuki, aliiambia Sabahi.
Alisema wenye siasa kali za kidini kwa pande zote mbili wanapaswa
kuhukumiwa binafsi na siyo kuonekana kama taswira ya dini ya imani hiyo
yote. "Kwa nini jamii kubwa inasumbuliwa kwa sababu ya vitendo au chuki
za mtu binafsi mmoja? Huo ni utovu wa hali ya juu wa ustahimilivu na
hatupaswi kuukubali," alisema.
Nyagah alilalamikia shambulio la guruneti la terehe 30 Septemba ambalo
lilimuua mtoto mmoja na kujeruhi watu wengine tisa katika kanisa la
Anglikani la Mtakatifu Polycarp katika wilaya ya Pangani jijini Nairobi,
pamoja na vitendo vya vurugu vinavyowalenga wenye asili ya Kisomali
baada ya mlipuko huo.
Comments