Skip to main content

Na Gazeti la NIPASHE: Tume ya Warioba kutafuna bilioni 40/-





Na Mwandishi wetu 24th June 2012

- Kwa mwaka kila mjumbe kuvuna zaidi ya milioni 300/-
– Wasio wajumbe yaani watumishi kutumia bilioni 4.3/-
– Sh bilioni 2.0 kulipia nyumba wafanyakazi wa Sekretariati

Serikali imefanya kufuru ya kutenga Sh. bilioni 40/- kwa ajili ya wajumbe 34 wa Tume ya Kuratibu Maoni ya Katiba. Kwa mujibu wa kasma ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliyoko kwenye Bajeti ya Serikali ya mwaka 2012/13.

Iliyopewa jina la Vote Number 8 (Fungu namba 8), wajumbe 34 wa tume hiyo wametengewa posho ya Sh. bilioni 10 watakayolipwa kwa kipindi cha mwaka mmoja jambo ambalo baadhi ya wabunge wamesema hawaridhiki na kuhoji serikali inatafuta kitu gani kwa tume hiyo.

Wajumbe wa kawaida wa tume hiyo kwa mujibu wa mchanganuo wa bajeti, watalipwa posho ya Sh. karibu 450,000 kwa siku lakini Makamu Mwenyekiti na Mwenyekiti wa Tume fungu lao ni kubwa zaidi ambalo limeongezewa viburudisho na takrima.

Kwa mujibu wa taarifa za uchambuzi wa posho hizo, kila mjumbe kuanzia mwaka wa fedha wa Julai 2012 hadi Julai 2013, atakuwa amejikusanyia zaidi ya Sh milioni 294 jambo ambalo baadhi ya wabunge waliohojiwa na NIPASHE Jumapili walisema ni maajabu ya Firauni.

Pamoja na kuhakikishiwa kuwa na ukwasi mkubwa, pia wametengewa Sh. milioni 10 kwa ajili ya matibabu kwa wale ambao wameelezwa kuwa hawapo kwenye utaratibu wa kugharamiwa tiba na serikali.

Dau kubwa ambalo lipo kwenye bajeti hiyo kwa mujibu wa wabunge hao ambao wameomba majina yao yasitajwe, ni kutengwa Sh. milioni 250 zinazodaiwa zitatumika kwa ajili ya usafi na ulinzi wa ofisi za Tume ya Mabadiliko ya Katiba.

Comments