| Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta |
Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta ameahidi kuwa, serikali yake itaendelea
kuheshimu na kulinda uhuru wa wanahabari pamoja na vyombo vya habari
nchini humo.
Akizungumza leo wakati wa kufungua rasmi mkutano wa kimataifa wa
waandishi wa habari mjini Nairobi, Rais Kenyatta amesema sekta ya
uandishi habari ni kiungo muhimu katika jamii na kwa mantiki hiyo
amevitaka vyombo vya habari kuwajibika zaidi kwa manufaa ya Wakenya.
Rais wa Kenya aidha ameonya vyombo vya habari ambavyo hutumiwa na
wanasiasa kuchochea fujo na machafuko kwamba serikali yake haitasita
kuvichukulia hatua kali za kisheria.
Ametoa mfano wa mauaji ya kimbari ya Rwanda ya mwaka 1994 ambayo
yalichochewa zaidi na vyombo vya habari na kusema serikali
haitowavumilia wenye nia ya kuivuruga nchi.
Mkutano huo wa kimataifa unawashirikisha wanahabari kutoka nchi
mbalimbali duniani na unatarajiwa kumalizika hapo kesho wakati dunia
itakuwa inaadhimisha siku ya kimataifa ya kutetea uhuru wa wanahabari.
Comments