Mashabiki wa Bayern Munich walisherehekea kipigo cha pili katika muda wa
siku tisa dhidi ya timu ya Barcelona iliyotamba na usakataji wake wa
soka katika bara la Ulaya na pengine dunia, ilipokubali kipigo cha mabao
3-0.
Barcelona ilichezea kipigo cha mabao 4-0 mjini Munich Jumanne iliyopita
na kipigo cha jana (01.05.2013), kinaashiria kuwa huenda utandazaji wa
soka wa kile kinachojulikana kama " tiki taka" , unaelekea ukingoni.
Bayern Munich ilivamia ngome ya Nou Camp na kufanikiwa kupata nafasi ya
kuingia katika fainali ya kwanza ya timu mbili za Ujerumani katika
kinyang'anyiro cha Champions League. Bayern imekamilisha hatua hiyo kwa
kipigo cha jumla ya mabao 7-0 dhidi ya barcelona, na kuingia katika
daraja la kuitwa wafalme wapya wa Ulaya.
Mabingwa hao wapya wa Bundesliga , ambao wanafukuzia ubingwa wao wa tano
katika mashindano hayo ya bara la ulaya , watapambana na Borussia
Dortmund hapo Mei 25 katika uwanja maarufu wa Wembley mjini London.
Messi aduwaa
Nyota wa Barcelona Leonel Messi alikuwa akitazama tu akiwa benchi wakati
Bayern ilipokamilisha dhoroba yake na kuwasambaratisha mabingwa hao
watarajiwa nchini Uhispania kwa mabao 3-0.
Kwa kumuweka benchi mfungaji wao huyo maarufu baada ya kupata maumivu ya
paja , Barcelona walishindwa kuipa changamoto ya maana Bayern, na
kushindwa kufurukuta kuweza kupindua matokeo ya hapo awali ya mabao 4-0
mjini Munich.
Comments