Skip to main content

Kukosekana kwa viwango vya elimu kikanda kunazuia ukuaji wa biashara katika Afrika Mashariki




Na Rajab Ramah, Nairobi
Kushindwa kutekeleza mfumo wa elimu ya kawaida yenye sifa zilizowekwa katika kiwango kilichokubalika ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kumezuia mtiririko wa fursa za rasilimali watu na biashara, wadau wasema.
Mhandisi wa Kampuni ya Kuzalisha Umeme ya Kenya akisimamia mifumo katika chumba cha kudhibiti umeme unaozalishwa kutokana na maji ya bwawa. Kwa kuwa na viwango vya elimu vyenye uwiano, wahandisi wangeweza kufanya kazi katika nchi za Afrika Mashariki ambazo zina uhitaji mkubwa. [Tony Karumba/AFP]
"Kila nchi ina viwango tofauti katika kuajiri wafanyakazi kwa sababu ya kutofautiana kwa mfumo wa elimu," alisema Patrick Obath, mjumbe wa Baraza la Biashara la Afrika Mashariki, asasi mama ambayo inawezesha ushiriki wa sekta binafsi katika mchakato wa kujumuisha EAC.
"Jambo hili linazuia uwezo wa kuwepo, mfano, raia wa Uganda kufikiriwa katika kazi nchini Kenya au Tanzania na kinyume chake," aliiambia Sabahi. "Hili linazuia utekelezaji wa itifaki ya soko la pamoja."
EAC, makao makuu yako Arusha, Tanzania, ni asasi baina ya serikali ambayo inadhamiria kupanua ujumuishaji wa kiuchumi, kisiasa na kiutamaduni baina ya Burundi, Kenya, Rwanda, Tanzania na Uganda.
Obath alisema kushindwa kurahisisha fursa za ajira nje ya mipaka kumefanya mchakato wa ujumuishaji wa EAC na ushindani wa kikanda kwa ujumla kwenda taratibu.

Comments