Skip to main content

Vita mpya ya CCM, CHADEMA bungeni


MWENENDO wa Bunge la Bajeti linaloendelea mjini hapa, umebaini kuwa vita ya maneno, fitna kati ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), sasa imehamia bungeni, Tanzania Daima Jumatano limebaini.
Moto wa vita hiyo kati ya vyama hivyo hasimu, umekolezwa zaidi baada ya Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais Jakaya Kikwete kufanya mkutano wa kimkakati na wabunge wa chama chake mjini hapa.
Duru za siasa kutoka ndani ya kikao hicho cha wabunge na rais, zilieleza kuwa Rais Kikwete aliwataka wabunge hao wa CCM wajipange kukabiliana na hoja za CHADEMA ambazo katika siku za hivi karibuni zimeonekana kulitikisa Bunge kiasi cha kiti cha spika kuamua kutumia kanuni kandamizi kuzizima.
Wabunge wa CCM bila kujali uzito wa hoja, wameamua kukabiliana na hoja zozote za wabunge wa CHADEMA hata kama zina maslahi kwa taifa.
Tayari CHADEMA kimeeleza kubaini mbinu hizo, kikidai kuwa hata kitendo cha Spika Anne Makinda kukatisha hotuba ya msemaji wao katika Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Joseph Mbilinyi ilikuwa sehemu ya utekelezaji wa mkakati huo.
Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa CHADEMA, John Mnyika alisema kuwa hatua hiyo ndiyo iliwafanya wasikubali kubadili hotuba yao hiyo kuanzia ukurasa wa kwanza hadi wa 14 kama ilivyotakiwa na spika kwani ni kinyume na kanuni ya 63 (2).

Comments