Skip to main content

Kongamano la kutoa taswira muelekeo katika ushiriki wa watu wote katika uchumi wa viwanda lafanyika




Watafiti wa masuala ya Biashara kutoka Afrika Mashariki wamesema nchi wanachama wanapaswa kuandaa mazingira wezeshi kwa wahitimu wa vyuo vikuu ili waweze kushiriki kikamilifu katika uchumi wa viwanda.

Wito huo umetolewa na washiriki wa Kongamano la Utafiti wa Biashara na viwanda lililofanyika katika Shule ya Biashara  ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam jana.

Akitoa ufafanuzi kuhusu kongamano hilo Dk.Ambroz Ntika Mkuu wa Kurugenzi ya Biashara na Ujasiriamali wa shule ya Biashara Chuo Kikuu cha Dar es salaam alisema kongamano hilo litatoa muelekeo katika ushiriki wa watu wote katika uchumi wa viwanda.

“Serikali iandae mazingira wezeshi ambapo wanafunzi wetu kuanzia ngazi ya chini wanapohitimu waweze kujitegemea na siyo kusubiri kuajiriwa kwakufanya hivyo tutatengeneza ajira nyingi na pato la kaya na Taifa litaimarika,’alisema.

Washiriki wa Kongamano hilo watadadavua mada 12 muhimu nakuzitolea maamuzi nakuzipeleka kwa watunga sera katika serikali za nchi wananchama ili kufanyiwa kazi ambapo mada 35 zitawasilishwa.

Dk.Ntika alisema mkutano huo kwa Tanzania umekuja wakati muafaka ambapo zaidi ya viwanda 3000 vya kati na vidogo vimeanzishwa ndani ya miaka mitau ya utawala wa Rais Dk. John Pombe Magufuli.

Kwa upande wake Profesa Isaack Mbeche kutoka shule ya Biashara Chuo Kikuu cha Nairobi alisema wamekutana ili kuchambua tafiti walizozifanya nakuziwasilisha katika idara mbalimbali kwa nchi wanachama ili zifanyiwe kazi.

Hata hivyo Uhuru lilitaka kujua je tafiti hizo zinafanyiwa kazi ipasavyo au zinakusanywa na kisha kuwekwa kwenye kabati,akijibu swali hilo Profesa Mbeche alikiri kuwa kuna uzembe katika serikali za nchi wanachama kwa kisingizo cha kukosekana rasilimali fedha.

“Ni ukweli usiopingika kuwa tunaandika maandiko mengi na tafiti nyingi lakini suala la utekelezaji lina kuwa na ukwakwasi na wakati mwingine shida haipo mamlaka za juu lahasha utakuta mkuu wa idara anakwamisha utekelezaji bila sababu za msingi zaidi atakuambia fedha hakuna.

Hata hivyo Profesa Mbeche alishauri ili tuweze kuimarisha viwanda vya ndani nchi wanachama hawana budi kulinda viwanda hivyo kwakununua bidhaa za ndani na kupenda bidhaa za nchi wanachama lakini wakitakiwa kuzalisha bidhaa zenye ubora.

Mmoja wa washiriki wa Kongamano hilo ambaye pia ni mwanafunzi wa mwaka watatu akichukua shahada ya Biashara chuoni hapo Geoffrey Mwamanga aliliambia Uhuru ili soko la ndani na viwanda viweze kushamiri sula la sarafu moja na soko la pamoja ni muhimu kwa wakati huu.

“Kinadharia tunaambiwa kuna soko la pamoja limeanza lakini binafsi sioni kimatendo kwakua hatuna sarafu moja kama wenzetu huko ulaya hapa nnachoshudia ni makongamano tu na maonesho ya kimataifa ya Biashara mara jua kali au sabasaba,”alisema.

Kongamano hilo ni la 14 kufanyika nchini na Kongamano linguine litafanyika nchini Uganda mwaka 2019.

Comments