Skip to main content

Niyonzima Kikosini kuusaka ubingwa Simba

Simba inahitaji pointi tano tu kutangaza ubingwa wa Ligi Kuu na kiungo wao Mnyarwanda Haruna Niyonzima 'Fabregas' aliyekosa mechi dhidi ya Yanga, amerudi kuungana na wenzake na kupigania ubingwa huo waliukosa kwa takribani miaka mitano.

Niyonzima amerudi akitokea kwao Rwanda alipokuwa kwenye msiba wa dada yake anayeitwa Sumaye jambo lililomsababishia akakosa mchezo  dhidi ya Yanga mwishoni mwa mwezi uliopita.
Amerudi na kukuta timu yake inahaha kusaka pointi tano ambazo zitawatangaza kuwa mabingwa msimu huu na hiyo ni baada ya kucheza mechi 26 na kuvuna pointi 62 sasa wanahitaji hizo tano ili wafikishe 67 ambazo hazitafikiwa na timu nyingine yeyote.
Yanga ndiyo timu pekee wenye nafasi ya kuwapindua Simba kama watapoteza mechi zao baada ya kucheza mechi 24 na kufikisha pointi 49, wakishinda mechi zao zote sita zilizobaki watakuwa na 66 na ndiyo nafasi yao pekee.
Kwani Azam inayowafuata nyuma, wao wameshautema rasmi ubingwa huo kwa sababu mechi 26 walizocheza wamepata pointi 49, hata wakishinda  zote nne zilizobaki watakuwa na 61 tu.
Meneja wa Simba, Richard Robert amesema: "Haruna amesharudi na kuungana na wenzake kwenye timu kwa ajili ya maandalizi ya michezo mingine ijayo. Ameshaanza mazoezi na wenzake na kila kitu kinakwenda sawa."

Comments