Skip to main content

Na Gazeti la Mwananchi: Kampeni kali yaanza dhidi ya Kenyatta, Ruto


Ruto anataka asilimia 50 ya nyadhifa hizo na amemwambia Kenyatta kwamba atagawa nyadhifa zilizosalia na vyama vingine katika muungano huo kama vile New Ford Kenya ya Eugene Wamalwa na Narc ya Charity Ngilu.
MGOMBEA Urais wa Kenya, Uhuru Kenyatta amekuwa katika ziara zisizokoma za nchi za Afrika Mashariki kwa lengo la kutafuta uungwaji mkono wa marais wa nchi hizo.
Tayari amekutana na kufanya mashauriano na viongozi wa Tanzania, Burundi, Sudan Kusini miongoni mwa wengine, na bado anaendelea na ziara hizo.
Huku nyumbani, baadhi ya viongozi na wagombea wa urais kama vile Naibu Waziri Mkuu, Musalia Mudavadi na Martha Karua wanatoa onyo kali na ushauri kwa Wakenya wasidhubutu kuwachagua washukiwa hao wasije wakajuta.
Mudavadi anasema kwamba Wakenya wakifanya makosa ya kuwapa Kenyatta na William Ruto jukumu la kuwaongoza, nchi itakuwa katika mashaka makubwa katika nyanja za kiuchumi na kisiasa ulimwenguni. Kiongozi huyu hapo awali alikuwa akiunga mkono wawili hao na hata kuwaambia Wakenya kuwa mzigo wanaobeba viongozi hao katika Mahakama Kuu ya Kimataifa ya ICC huko The Hague, Uholanzi, ni mzigo wa Wakenya wote.
Makamu wa Rais, Kalonzo Musyoka kwa kuwa bado anatarajia kwamba kuna uwezekano wa kuwa katika muungano na washukiwa hao, haswa Ruto, hataki kamwe kugusia suala hili. Juzi, katika mkutano wa kisiasa, aliukejeli muungano ambao sasa unayumbayumba kati ya Kenyatta na Ruto. Mazungumzo ya muungano kati ya viongozi hao wawili yamepigwa na dhoruba kali kwa sababu hawajakubaliana kuhusu nyadhifa za mawaziri na maspika wa Bunge na Seneti.

Comments