Skip to main content

CCM yajipima kwa CHADEMA


VIGOGO WAPYA, MAWAZIRI KUANZA ZIARA MIKOANI
KATIKA mikakati yake ya kupambana na nguvu za operesheni za CHADEMA mikoani, Chama cha Mapinduzi (CCM), kimelazimika kuwatumia viongozi wake wapya wakiongozana na mawaziri ili kwenda mikoani kufafanua kwa wananchi jinsi serikali ilivyotekeleza ilani yake.
Hii itakuwa ni mara ya pili kwa chama hicho kujaribu kukabiliana na upinzani wa CHADEMA mikoani, ambapo mwaka jana baada ya mkutano wao wa maazimio ya kujivua gamba, walijitahidi kuzunguka baadhi ya mikoa bila kufua dafu.
Operesheni zinazofanywa na CHADEMA za Sangara na sasa Vuguguvu la Mabadiliko (M4C), zimeitikisa CCM na hivyo wajumbe wake kutumia muda mwingi kwenye mkutano mkuu wao uliomalizika mjini Dodoma, kujitapa kuwa lazima wafanye mashambulizi ya kuwasambaratisha.
Akitangaza mkakati huo mpya jana kwa waandishi wa habari wa kuchanja mbunga kwa kutumia anga kwa helikopta kama CHADEMA, Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alisema wameanda ziara ya siku nne katika mikoa minne.
Alisema ziara hiyo itaongozwa na sekretarieti mpya chini ya Katibu wake Mkuu, Abdullahman Kinana, na kuwashirikisha baadhi ya mawaziri.
Nape alisema kuwa ziara hiyo ni ya chama na sio ya kiserikali na kwamba itaanza kesho hadi Novemba 24 katika mikoa ya Mtwara, Arusha, Geita na Rukwa.
Akifafanua zaidi alisema Kinana ataanzia Mtwara ambako atakuwa na mawaziri husika wanaoshughulikia masuala ya kilimo ili kuzungumzia zao la korosho na waziri wa uchukuzi atakayezungumzia bandari na miundombinu.

Comments