Skip to main content

Minziro kutibua sherehe Yanga leo?

Fred Felix Minziro
Yanga inaumana na JKT Ruvu ya Fred Felix Minziro leo kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, lakini ni kocha mkuu wa kikosi hicho cha wanajeshi anayeweza kutibua hesabu za mwenzake wa Yanga, Hans Pluijm kusaka ubingwa.
Minziro aliyekulia na kucheza soka Yanga kwa maisha yake yote ya miaka 13, aliinoa timu hiyo kabla ya kutimuliwa, anakutana nayo (Yanga) ikiongoza ligi ikiwa na pointi 37 na kufuatiwa na Azam yenye pointi 36 na Simba ni ya tatu ikiwa na pointi 32.
Kocha huyo alisema Yanga wasitarajie mteremko kwao na watakomaa nao leo kuhakikisha wanaondoka na pointi tatu.
"Tuko vizuri na Yanga wasitarajie mteremko kwetu, tutacheza kwa kiwango kikubwa kuhakikisha tunaibuka washindi, najua ni timu nzuri na inaongoza ligi lakini hata sisi tuko pabaya tunahitaji kujinasua na kupanda nafasi za juu ili kukwepa kushuka daraja," alisema Minziro.
Kwa upande wake, Pluijm amekiri kuwa hautakuwa mchezo rahisi kuikabili JKT Ruvu ambayo ni timu ngumu kama ilivyo ligi yenyewe.
Timu hiyo hivi inaikabili JKT Ruvu ikiwa na presha kwani inahitaji ushindi kwa hali yoyote ile kutokana na wapinzani wao, Azam kuwafuatia kwa karibu.
Pluijm aliliambia gazeti hili kuwa wamejiandaa vizuri, ingawa haitakuwa kazi rahisi kwao kupata ushindi mbele ya wanajeshi hao kwani ligi ni ngumu hivi sasa na kila timu iko katika kiwango kizuri.
Alisema amewaelekeza wachezaji wake kuichukulia kwa umakini mkubwa michezo yote iliyobaki ili waweze kushinda na kutwaa ubingwa.
"Ligi ni ngumu na kila timu imeonyesha uwezo mkubwa na ndiyo maana nasema haitakuwa kazi rahisi kushinda dhidi ya JKT Ruvu, lakini tumejiandaa, wachezaji wangu wako katika kiwango kizuri na naamini tutapata pointi zote tatu.
"Kikubwa ni kushinda kila mechi iliyo mbele yetu, hatuhitaji kupoteza chochote maana mpinzani wetu Azam anatufuatia kwa kasi hivyo lazima tupambane kuhakikisha kila mechi inakuwa kama fainali kwetu, nawaamini wachezaji wangu watafanya kazi nzuri na kuweza kupata ushindi kesho (leo)," alisema Pluijm.
Hata hivyo, Yanga itamkosa mshambuliaji wake mahiri, Amissi Tambwe mwenye kadi tatu za njano, kiungo Andrey Coutinho aliye majeruhi pamoja na Jerryson Tegete anayesumbuliwa na maumivu ya bega.
Mrisho Ngassa aliyekuwa na maumivu ya nyama za paja na kuukosa mchezo uliopita dhidi ya Mgambo Shooting amerejea kikosini na kufanya mazoezi na wenzake jana asubuhi, ingawa daktari wa timu hiyo Juma Sufiani alisema watamwangalia atakavyoamka leo ili kujua maendeleo yake na kama atacheza mchezo wa leo au la.
Hata hivyo, pia kiungo Said Juma Makapu aliyezimia uwanjani dakika za mwisho katika mchezo dhidi ya Mgambo amerejea na kufanya mazoezi na wenzake jana asubuhi.
JKT Ruvu itamkosa Zubery Napho ambaye alipata maumivu katika mazoezi wakati ikijiandaa kuikabili Ndanda wiki iliyopita.
Chanzo:Mwananchi

Comments