Skip to main content

Kenya nao kutumia ndege zisizo na marubani kuzuia waingizaji wa silaha za magendo, al-Shabaab


Na Bosire Boniface, Garissa
Kenya inajiandaa kusambaza ndege zisizo na marubani aina ya 'drones' kama sehemu ya operesheni za usalama zilizoongezwa katika mipaka yake na Somalia na Ethiopia kufuatilia na kukomesha harakati za al-Shabaab na waingizaji wa silaha za magendo, maofisa usalama waliiambia Sabahi.


Vikosi vya usalama vya Kenya vikifanya misheni ya ukaguzi huko Liboi katika mpaka wa Kenya na Somalia mwezi Oktoba 2011 baada ya wafanyakazi wawili wa msaada wa Kihispania kutekwa katika kambi ya wakimbizi ya Dadaab. [Tony Karumba/AFP]
Ndege aina ya 'drones', au vyombo vya angani visivyo na marubani, zinahitajika kusaidia vikosi vya usalama vya Kenya kufanya doria katika mipaka ya nchi, alisema Patrick Ochieng, mkurugenzi wa Eneo Lengwa La Kitaifa la Kenya kuhusu Silaha ndogondogo na Silaha Nyepesi.
"Tunakabiliwa na changamoto za ulinzi ambazo hazijawahi kutokea," aliiambia Sabahi. "Sio tu kuwa tuna vitisho kutoka ndani ya nchi, bali pia kutoka kwa waasi wa al-Shabaab."
Uingizaji silaha kwa magendo na upenyezaji unaofanywa na al-Shabaab katika mkoa wa kaskazini-mashariki wa Kenya umeleta hali ya kutokuwa na usalama pamoja na athari mbaya, alisema, akiongeza kwamba miaka miwili iliyopita imeshuhudia ongezeko la vurugu kutokana na bunduki haramu, kwa wahalifu na wauza silaha kwa magendo kuzua njia mpya za kuuza silaha kwa magendo.
Polisi wa Kenya wenye hadhi ya kijeshi jijini Nairobi wakilichoma rundo hili la silaha haramu zilizokamatwa mwezi Machi 2009. [Simon Maina/AFP]

Ndege zisizo na marubani zitawekewa teknolojia ya kiwango cha juu ikiwa ni pamoja na kamera zinazoweza kuona usiku ili kuisaidia Kenya kuwashinda wahalifu na kuondoa vitisho vya usalama, Ochieng alisema.
Maofisa usalama wanapata mafunzo kuhusu ndege zisizo na marubani, ambazo zitaanza kazi mwishoni mwa mwaka huu, alisema Ochieng. Alikataa kupeana maelezo zaidi kuhusu programu hiyo, alisema kwamba kwa kufanya hivyo kutasaidia wanaoingiza silaha nchini.

Comments