Skip to main content

Vurugu Chadema: Mwigamba apinga kusimamishwa,Mnyika apigilia msumari hukumu hiyo


Arusha. Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Arusha, Samson Mwigamba, amepinga uamuzi wa kusimamishwa kwa maelezo kuwa kikao kilichochukua uamuzi huo hakitambuliki kikatiba huku akikanusha tuhuma za kutumiwa na Naibu Katibu Mkuu, Zitto Kabwe, kukisambaratisha chama hicho.

Hizi tuhuma kuwa natumiwa na Zitto nimekuwa nikizisikia, lakini huo ni upofu, mimi si mtu wa kutumika nina elimu yangu nzuri ya shahada ya kwanza ya utawala wa biashara, najua ninachokifanya ni kwa masilahi ya chama. Samson Mwigamba
Akizungumza jana na gazeti hili, Mwigamba alisema kikao ambacho kina mamlaka ya kumwajibisha ni Kamati Kuu baada ya kupokea tuhuma na kumsikiliza.
“Baraza la uongozi la Kanda halina mamlaka ya kunisimamisha uenyekiti, lakini kwa kuwa mimi bado ni mwanachama hai wa Chadema na sitahama Chadema, nitakaa pembeni ili chama kifanye uchunguzi wa tuhuma zangu nikiwa nje ya ofisi,” alisema Mwigamba.
Hata hivyo, alisema anakusudia kufafanua chanzo cha mgogoro wake na baadhi ya viongozi leo, baada ya kukabidhiwa kompyuta mpakato (laptop) na viongozi wa chama hicho ambao waliichukua ili kuifanyia uchunguzi.
Akana kutumiwa na Zitto
Akizungumzia tuhuma za muda mrefu kuwa, amekuwa akitumiwa na Zitto hasa kuelekea uchaguzi ndani ya chama hicho, alisema wanaofikiri hivyo ni vipofu wa kisiasa.
“Hizi tuhuma kuwa natumiwa na Zitto nimekuwa nikizisikia, lakini huo ni upofu, mimi si mtu wa kutumika nina elimu yangu nzuri ya shahada ya kwanza ya utawala wa biashara, najua ninachokifanya ni kwa masilahi ya chama,” alisema Mwigamba.

Comments