Skip to main content

Mali inataka msaada wa jeshi la kimataifa kuidhibiti sehemu ya kaskazini


Mkutano wa Umoja wa Mataifa New York
Mali imeuomba Umoja wa Mataifa utoe kibali cha haraka kwa jeshi la kimataifa liisaidie serikali ya nchi hiyo izidhibiti tena sehemu za kaskazini ya nchi hiyo.
Habari hiyo imetolewa na waziri wa mambo ya kigeni wa Ufaransa, Laurent Fabius.
Nchi hiyo ya Afrika magharibi ilitumbukia katika michafuko mwezi Machi mwaka huu, pale wanajeshi walipompindua kutoka madarakani rais, hivyo kuweko pengo wazi la madaraka. Hali hiyo iliwawezesha waasi wa Ki-Tuareg kutwaa thuluthi mbili ya nchi hiyo. Lakini makundi ya kiislamu, baadhi yao yakiwa na ushirikiano na mtandao wa Al-Qaeda, yaliuteka nyara uasi huo katika sehemu za kaskazini ya nchi na kuanzisha kutekelezwa sheria za kiislamu.
Akiiashiria barua iliopelekwa na viongozi wa mpito wa Mali kwa katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon, hapo Septemba 18, Laurent Fabius alisema Mali imeomba lipitishwe azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa chini ya Ibara ya Saba ya Hati ya Umoja huo ili kutolewe kibali cha kutumiwa jeshi la kimataifa lilisaidie jeshi la Mali kuyateka tena maeneo ya kaskazini mwa Mali. Ibara hiyo ya Saba inaliruhusu baraza la usalama litoe kibali cha kuchukuliwa hatua kutoka zile za kibalozi na za kiuchumi hadi kujiingiza kijeshi.
Laurent Fabius, akiisoma barua hiyo, aliwaambia waandishi wa habari kwamba kwa miezi kadha Mali imekuwa ikikabiliwa na mzozo wa usalama usiowahi kuonekana kabla katika maeneo yake ya kaskazini ambayo yametawaliwa na makundi yenye silaha, wakiwemo magaidi, wasafirishaji wa mihadharati na aina zote za wahalifu. Alisema serikali ya Mali inataka jeshi la aina hiyo lipelekwe kwa haraka ili kuyasaidia majeshi ya usalama ya Mali kutekeleza shughuli hiyo.

Comments