Skip to main content

Al-Shabaab wakaribia kuipoteza Kismayo

Wanajeshi wa Ethiopia karibu na mji wa Kismayo.
Jeshi la Umoja wa Afrika nchini Somalia (AMISOM) pamoja na Jeshi la Kenya wamethibitisha kupambana na wanamgambo wa al-Shabaab ndani ya mji wa bandari wa Kismayo, wakidai kukaribia kuuchukua mji huo muhimu kimkakati.
"Lengo la AMISOM ni kuwakomboa watu wa Kismayo na kuwawezesha kuendelea na maisha yao kwa amani, utulivu na usalama. Operesheni zetu zinaendelea kulenga shabaha maalum za al-Shabaab mjini Kismayo," alisema Kamanda Andrew Gutti wa AMISOM, akiwataka wapiganaji wote wa al-Shabaab walio ndani ya Kismayo kuweka chini silaha zao.
Katika hatua nyengine, Jeshi la Kenya limesema kwamba wapiganaji wake wamelichukua eneo la kusini ya Kismayo, ngome ya mwisho ya kundi la al-Shabaab.
Msemaji wa Jeshi hilo, Cyrus Oguna, aliliambia shirika la habari mapema leo kwamba wanajeshi wa Kenya walikumbana na upinzani mdogo wakati wa kuliteka eneo hilo.
Al-Shabaab, wakaazi wa Kismayo wakanusha
Hata hivyo, wakaazi wa huko pamoja na wanamgambo wa al-Shabaab wamekanusha taarifa hizo, wakisema kwamba ndio kwanza wanajeshi wa Kenya walikuwa kwenye viunga vya mbali na Kismayo, ambako wamekuwako kwa zaidi ya siku nne sasa.

Comments