Skip to main content

Viongozi wa dini Tanzania wataka uvumilivu baada ya ghasia ya kidini


Na Deodatus Balile, Dar es Salaam
Viongozi wa dini nchini Tanzania wamelaani wimbi lililoibuka hivi karibuni la machafuko yanayotokana na tofauti za kiimani kati ya Wakristo na Waislamu ambayo tayari yameshasababisha vifo vya viongozi watatu katika kipindi cha mwezi Februari, na kuapa kuzirejesha jamii hizi mbili katika hali ya kawaida.
Baadhi za viongozi hao wanasema kuwa mahubiri yanayotelewa bila kuwa na kibali husika kwenye makanisa na misikiti ndio kiini cha hali ya mtafaruku inayoendelea sasa. Juu, wanaume wakifanya ibada msikitini jijini Dar es Salaam. [Na Mwanzo Millinga/AFP]
Tarehe 11 Februari, mzozo kati ya wafuasi wa dini hizo mbili juu ya nani anafaa kuchinja nyama ulisababisha kifo cha mchungaji Mathayo Machila aliyekuwa na umri wa miaka 45 na kusababisha wananchi wengine kujeruhiwa. Tangu wakati huo serikali imeanzisha kamati ya viongozi wa dini kwa lengo la kurejerea sheria za kiimani kuhusu kuchinja mifugo mbalimbali kwa ajili ya nyama.
Visiwani Zanzibar, Mchungaji Evarist Mushi aliuawa kwa kupigwa risasi na watu wasiojulikana nje ya kanisa lake tarehe 17 Februari, wakati pia tarehe 23 Februari Sheikh Ali Khamis Ali, 65, aliuawa na watu wasiojulikana kwenye shamba lake la minazi.
Mauwaji hayo ya mwezi Februari ni mwendelezo wa matukio yaliyoanza mwaka uliopita. Katika sherehe za Krismasi, watu waliokuwa na silaha walimshambulia kwa risasi Mchungaji Ambrose Mkenda wakati alipokuwa njiani akirejea nyumbani, na mwezi Novemba watu wasiojulikana walimshambulia kwa kumwagia tindikali Sheikh Fadhil Soraga.
Sheikh Mkuu wa Tanzania, Mufti Issa Bin Shaaban Simba, amesema kuwa nchi inatakiwa kuhamasisha uvumilivu wa kidini.
"Tumekuwa tukivumiliana kwa muda mrefu lakini sasa uvumilivu huo umekwenda wapi?" aliiambia Sabahi. "Serikali, viongozi wa dini na wanasiasa wanapaswa kuhubiri amani, upendo na utulivu."

Comments