Skip to main content

Bei ya umeme kushuka Machi


Mkurugenzi mkuu wa mamlaka ya udhibiti wa nishati, maji nchini Felix Ngalamgosi akizungumza na waandishi wa habari
Mkurugenzi mkuu wa mamlaka ya udhibiti wa nishati, maji nchini Felix Ngamlagosi akizungumza na waandishi wa habari
Serikali imeshusha bei ya umeme nchini kwa asilimia 2.21 kuanzia mwezi Machi mwaka huu.
Bei hiyo itatumika katika kipindi cha miezi mitatu wakati mapitio mapya yakiwa yanafanyika kulingana na mfumuko wa bei.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Udhibiti wa huduma za Nishati na Maji (Ewura), Felix Ngamlagosi, alisema hatua hiyo imekuja baada ya kupitia gharama ya uzalishaji wa umeme kwa kuzingatia mabadiliko ya bei ya mafuta, thamani ya shilingi ya Tanzania na mfumuko wa bei.
Alisema  kufuatia bei hiyo mpya watumiaji wa majumbani  wamepunguziwa kwa shilingi nane kutoka Sh. 306 hadi Sh. 298.
Watumiaji wa kati wanaotumia umeme wa Volti 400, bei itashuka kutoka Sh. 205 hadi Sh. 200 kwa uniti moja, sawa na punguzo la Shilingi tano kwa uniti.
Wateja wakubwa walionganishwa katika msongo wa kati wa umeme, watapunguziwa kwa Shilingi nne, ambapo watanunua Sh. 159 badala ya Sh. 163 ya awali.
Kwa wateja waliounganisha katika msongo mkubwa wa umeme kama migodi na Shirika la Umeme Zanzibar, watapunguziwa Shilingi tatu, wamepunguziwa gharama kutoka Sh. 159 hadi Sh. 156 kwa uniti moja.
“Kwa wateja wa majumbani wenye matumizi madogo ya wastani wa uniti 75 kwa mwezi, bei ya umeme haitabadilika kutokana na kundi hilo kuchangiwa gharama na wateja wakubwa wa majumbani,” alisema.
Ngamlagosi alisema wateja hao wadogo wa majumbani wataendelea kulipia Sh. 100 kwa uniti moja.
Aidha akizungumzia namna walivyokokotoa gharama hizo, alisema katika kupindi hicho Tanesco iliokoa Sh. Bilioni 57 baada ya uzalishaji kuwa wa chini kwa mitambo ya uzalishaji inayotumia mafuta mazito na ya ndege..
Alisema katika kipindi hicho thamani ya shilingi ilishuka kwa wastani wa asilimia 7.28, wakati mfumuko wa bei uliongeza mahitaji ya pato la Tanesco kwa Sh. Bilioni 17.
Ngamlagosi gharama halisi ya pato la Tanesco kwa mwaka huo ulikuwa Sh. Bilioni 33.
Hata hivyo, alisema bei hiyo  itadumu kwa muda wa miezi mitatu baada ya kuwepo kwa kifungu cha kanuni kinachotaka bei elekezi katika huduma hiyo kubadilika kila mara.
Alisisitiza yapo matumaini ya kushuka zaidi kwa bei ya umeme baada ya kuanza kwa uzalishaji wa nishati hiyo kupitia mitambo ya Kinyerezi pamoja na kufanya marekebisho kwa mitambo iliyopo kutoka kuendeshwa kwa kutumia mafuta badala yake kutumia gesi.
Chanzo: NIPASHE

Comments