Skip to main content

Banda huyoooo Ifahamu zaidi Baroka FC

 


Na Salym Juma, Arusha
Nikinukuu kauli ya Abdi Banda katika maandishi kwamba, wachezaji wajitume na wanatakiwa kuwa makini na nafasi, hasa zinapotokea nafasi za kutoka kwenda kucheza nje ya nchi na wasiangalie nyuma. Kauli ya Beki huyu wa zamani wa Simba inawagusa Wachezaji ambao wanaamini Simba na Yanga ndio sehemu pekee ya mafanikio ambayo wanapaswa kufika. Ukweli ni kwamba hata hao akina Samatta na Ulimwengu walifika hapo walipo baada ya kuondoka Tanzania na kwenda kujaribu bahati zao nje.
Kufanya vizuri kwa Abdi Banda msimu uliopita kumemfanya mchezaji huyu kupata nafasi ya kusajiliwa na timu iliyoshiriki ligi kuu ya South Afrika msimu uliomalizika. Banda ambaye tayari alishasaini mkataba wa kujiunga na klabu hiyo wakati akiwa kwenye michuano ya COSAFA Cup 2017 iliyofanyika South Afrika anakwenda kucheza kwenye ardhi ya Mandela na kama akikitumia vyema kipaji chake huenda akapata shavu kwenye vilabu vikubwa vya South Afrika.
Banda ni aina ya wachezaji ambao hupenda sana kuuchezea mpira na mara nyingi hujaribu kupiga mashuti ya mbali langoni mwa mpinzani. Kitu cha msingi cha kuzingatia ni nidhamu kwani wachezaji wetu wanapaswa kuiga nidhamu ya akina Samatta au Himid Mao. Japo Banda amekuwa na nidhamu yenye mashaka na makosa ya hapa na pale ila naamini anao muda mzuri wa kurekebisha haya kabla ya kuanza kukipiga klabuni.
Watanzania wengi wanatamani kuijua kwa undani timu hii anayokwenda mchezaji huyu wa zamani wa Simba na Taifa Stars kwa sasa.
Baroka F.C ni klabu iliyopo South African inayotokea Ga-Mphahlele karibu na Polokwane, Limpopo. Timu hii ni miongoni mwa timu zilizoanzishwa hivi karibuni na imekuwa na mwenendo wa kuridhisha kadiri siku zinavyosonga. Tangu mwaka 2007 ilipoanzishwa ilijitahidi kupanda daraja kwenye msimu wake wa kwanza ila mechi ya mwisho kabisa iliwakwamisha baada ya kutoka sare na Thanda Royal Zulu. Baroka ni Timu changa ambayo inaweza kuwa na uhai mrefu huko tunapoelekea.

Comments