Skip to main content

Kura bado kitendawili Bunge la Katiba


Dodoma. Wakati wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba wakipitisha Rasimu ya Kanuni za kuendesha Bunge hilo, suala la aina ya kura kwa ajili ya kuamua masuala mbalimbali, limekwama na litaamuliwa na wabunge baada ya kuanza kwa vikao rasmi vya Bunge hilo.
Mjumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, Mchungaji Christopher Mtikila akimlalamikia Mwenyekiti wa muda wa Bunge hilo kwa kutompa nafasi ya kuchangia bungeni mjini Dodoma jana. Picha na Silvan Kiwale

Hatua hiyo imekuja baada ya kuwapo kwa mvutano wa takriban wiki nne kuhusu rasimu, hasa kifungu cha 37 na 38 kinachoeleza aina ya kura kati ya wazi na ya siri.
Hata hivyo, wajumbe wawili wa Bunge hilo, Mchungaji Christopher Mtikila wa DP na Felix Mkosamali wa NCCR- Mageuzi walisusia kupitisha azimio la kukubali Kanuni za Bunge hilo, wakidai kusalitiwa katika uamuzi huo na wenzao walioko kwenye Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Wajumbe na viongozi mbalimbali wa vyama vyenye ushawishi bungeni, kwa pamoja waliridhia na kulegeza misimamo yao ili upatikane mwafaka wa kutengeneza Katiba Mpya ndani ya wakati.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti ndani na nje ya Ukumbi wa Bunge mjini Dodoma, viongozi hao walisema masilahi ya Watanzania katika mchakato wa Katiba ni ya muhimu kuliko masilahi binafsi ya makundi.
Kinana asema
Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi, Abdulrahaman Kinana alisema pamoja na malumbano makali yanayoendelea katika Bunge la Katiba, anaamini sasa Katiba itapatikana.

Comments