Skip to main content

Tuukatae udikteta ndani ya vyama vya siasa



Monday, 19 December 2011 21:33

Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila
KATIKA hali inayotia mashaka kuhusu kukua kwa demokrasia katika vyama vya siasa hapa nchini, Chama cha NCCR-Mageuzi juzi kilitangaza kumvua uanachama Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila pamoja na makada wengine watatu katika kile kilichokiita kosa la kuzungumzia nje mambo ya ndani ya Chama, huku makada wengine 16, akiwamo mshirika wake wa karibu Mbunge wa Muhambwe,  Felix Mkosamali wakipewa onyo kali.
 
Hatua hiyo ya kushangaza ilitangazwa juzi na Katibu Mkuu wa chama hicho, Samwel Luhuza, ambaye alisema uamuzi huo ulitolewa na NEC  ya chama hicho baada ya kujadili tuhuma zilizotolewa na Kafulila na wanachama wengine ambazo zilijenga mtafaruku ndani ya Chama, hivyo kuwaona wana makosa na kuamua kuwavua uanachama. Mmoja wa makada  waliovuliwa uanachama ni aliyekuwa mgombea wa kiti cha urais wa chama hicho katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005 na 2010, Hashim Rungwe ambaye pia ni Mjumbe wa Baraza la Wadhamini wa chama hicho.
 
Ingawa hatuna nia wala mamlaka ya kuhoji au kupinga hatua hiyo iliyochukuliwa na chama hicho dhidi ya Kafulila na wenzake,  lazima tukiri waziwazi hapa kwamba hatudhani kama adhabu ya kuwafuta uanachama imechukuliwa kwa nia ya  kukijenga chama hicho, bali pengine  imechukuliwa ili kuwaziba midomo  waliokuwa wakiwakosoa viongozi wa chama hicho na kuficha chini ya zulia matatizo ya msingi.
Madai ya kwamba kosa la akina Kafulila limetokana na wao kuzungumzia masuala ya chama hicho katika vyombo vya habari ni la kinidhamu tu na pengine ni ushahidi tosha kuwa, chama hicho hakina muundo wa kidemokrasia kwa wanachama kujadili matatizo na kutoa dukuduku lao bila kunyamazishwa.
 
Moja ya hoja za akina Kafulila ambayo tunadhani ni ya msingi ni kwamba chama hicho kimedorora kwa sababu hakifanyi kazi ya siasa. Kazi ya chama cha siasa kilicho hai ni kupata viongozi wa kuhamasisha wanachama, kujenga chama kwa kufungua ofisi na matawi nchi nzima, kupata wanachama  wapya, kutoa elimu ya uraia,  kushiriki katika chaguzi mbalimbali katika ngazi zote na kuonyesha kwa vitendo nia na dhamira ya kutwaa dola.
Chama dhaifu na legelege hakina malengo wala dira, mbali na  viongozi kukaa ofisini na kusubiri ruzuku za serikali na michango ya wanachama.
 
Viongozi wa chama hicho walipaswa kujibu hoja na kuwatoa dukuduku wakosoaji kuhusu mustakabali wa chama chao badala ya awali kuandaa vikao vya siri na kula njama za kuwavua uanachama. Swali la kujiuliza hapa ni kama taratibu zilifuatwa, kwani tumeambiwa walikuwapo wajumbe 60 badala ya 40, huku wengine wakiwa hawafahamiki walikotoka. Ndiyo maana tunampongeza Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashililah aliyesema juzi kuwa, uamuzi wa chama hicho dhidi ya Kafulila utakubaliwa na Bunge iwapo demokrasia ilizingatiwa katika kufikia uamuzi huo.
 
Mchakato wa kuwapata wabunge ni mrefu na wenye gharama kubwa kwa taifa na walipakodi. Hivyo, haiwezekani mbunge avuliwe ubunge kienyeji na kirahisi tu kwa hisia na fununu za washindani wake mitaani au ndani na nje ya chama. Lazima ziwepo sababu na ushahidi wa kutosha dhidi ya mbunge kama ametenda kosa la jinai au hakuwajibika kwa wapigakura wake.
Tunakubaliana na Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa aliyekaririwa jana akisema kumvua mbunge uanachama kwa tuhuma zisizo na mashiko ni kusababisha kufanyika uchaguzi mdogo jimboni ambao unaligharimu taifa Sh19 bilioni.
 
Ni makosa makubwa kudharau michango ya wabunge vijana kama Kafulila katika Bunge hili la Kumi.  Kafulila ni mmoja wa wabunge waliovipatia vyama vyao heshima kubwa  bungeni kwa hoja za msingi zinazoweka mbele utaifa na uzalendo. Amepiga vita itikadi za vyama na uroho wa posho.
Katika kutambua hilo, NEC ya chama chake ingetumia busara kutumia kikao hicho kusameheana, hasa baada ya Kafulila kumwaga machozi mengi ya unyenyekevu kwa lengo la kuomba msamaha. Chanzo ni  Gazeti la Mwanachini.

Comments